A

A

WANANCHI WA KATA YA TANDALA MAKETE WAMBANA MBUNGE WAO KUHUSU KUTOWASHIWA UMEME WA GRIDI YA TAIFA


Ikiwa kata ya Tandala wilayani Makete mkoani Njombe ni miongoni mwa maeneo yanayosubiriwa kwa hamu kuwa na umeme wa gridi ya taifa, hivi karibuni wananchi wa kata hiyo wamembana mbunge wao aliyekuwa akipita eneo hilo na kumlalamikia kuhusu kutowaka kwa umeme.

Tukio hili limejiri hivi karibuni ambapo mbunge wa jimbo la Makete ambaye pia ni Waziri wa nchi ofisi ya makamu wa raisi anayeshughulikia mazingira Dkt Binilith Mahenge alikuwa akipita akitokea Dodoma kwa ajili ya kukabidhi sola katika shule ya sekondari Ikuwo, alikumbana na dhahama hiyo ambapo wananchi walisimamisha gari lake na kumtaka kuwasaidia kujua kulikoni umeme bado hauwaki katika kata hiyo licha ya nguzo na kila kitu kuwa tayari

"Mheshimiwa sisi tunashangaa mpaka sasa hakuna dalili za umeme kuwaka, nguzo zimefika kama unavyoona lakini umeme hauwaki, kila siku tunaambiwa mara tujiandikishe, mara vifaa havijaja, mara tusubiri kwanza na hela tushalipa, sasa tunajiuliza kwa nini mliharakisha kuleta umeme toka makete wilayani mpaka hapa kama mlikuwa hamna haraka ya kutuwashia?" alisikika Mwananchi mmoja akisema

Dkt. Mahenge amewatuliza wananchi hao kwa kuwaambia kuwa anasikitishwa na hali hiyo, huku akiwahakikishia kuwa umeme huo utawaka mara moja kama serikali ilivyokusudia

"Ndugu zangu wananchi naomba niwahakikishie mimi ni mbunge wenu, mmenituma kuwatumikia, nawahakikishia hili jambo litakwisha, nalikomalia hadi mwisho maana si lengo la serikali kuwa ninyi mpate tabu, umeme utawaka" amesema Dkt Mahenge

Kufuatia hali hiyo Waziri Mahenge amelazimika kuwasiliana na ofisi ya Tanesco wilaya ya Makete kujua sababu za wao kutowasha umeme katika kata ya Tandala ambapo alijibiwa na Meneja wa shirika hilo wilaya Bw. Zebedayo Gadau kuwa wananchi hawajachangia fedha kwa ajili ya wao kuunganishiwa umeme (Tsh. 175,000/=) na ndiyo maana wapo kimya

Bw. Gadau amesema umeme upo na transfoma zilizopo katani hapo zina umeme na kilichobaki ni kuunganisha kwenda kwa wananchi na hawawezi kufanya hivyo kama wananchi hawajalipia
Hali hiyo ilimfanya Dkt Mahenge kuomba kukutana na wananchi wa Tandala, Meneja Tanesco wilaya pamoja na yeye ili kujua utata uko wapi kwa kuwa maelezo ya meneja na wananchi hao yalikuwa tofauti ambapo ilibainika kuwepo kwa uzembe fulani katika ofisi ya Tanesco makete

Katika kikao hicho wananchi wamedai kuwa waliambiwa na Tanesco wafanye "wire ring" kwenye nyumba zao na shirika hilo lingekuja kukagua kabla ya kuwaunganishia umeme jambo ambalo walilifanya lakini baadaye waliwaambia wasilipe gharama za kuunganishiwa umeme kwanza mpaka watakapotaarifiwa

"Hilo halijafanyika mheshimiwa mbunge, mpaka sasa tunasubiri, sasa nashangaa tunavyoambiwa hatujalipia, je tutalipiaje ilihali tuliambiwa na tanesco tusubiri mapaka waje kutuambia, na hadi leo hii wapo kimya?" amesema mwananchi 

Kikao hicho kilimuamuru meneja huyo kuwaruhusu wananchi waje kulipia gharama za kuunganishiwa umeme ambapo agizo hilo lilipokelewa kwa furaha na wananchi hao

Hadi sasa wananchi wanaendelea kumiminika kwenye ofisi za Tanesco wilaya kulipia gharama hizo