Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk James Nzagi (kushoto)
akizungumza na waandishi wa habari kutoka Tanzania; Dismas Lyassa
(katikati) na Peter Saramba. Mazungumzo hayo yalifanyika ofisini kwake,
Bujumbura hivi karibuni. Picha na Filbert Rweyemamu.
Moja ya sababu kuu za kuanzishwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC),
ni kutoa wigo mpana wa soko na shughuli za kiuchumi miongoni mwa nchi
wanachama.
Tanzania na Burundi ni kati ya nchi tano zinazounda Jumuiya ya Afrika
Mashariki. Nchi nyingine wanachama ni Kenya, Uganda na Rwanda, wakati
nchi ya Sudan Kusini ikiwa imetuma maombi rasmi ya kujiunga.
Hivi karibuni, EAC iliandaa mafunzo ya siku tano kwa waandishi 25 wa
Ukanda huo, mafunzo yaliyoambatana na mkutano wa pili wa siku tatu
kuhusu Amani na Usalama miongoni mwa nchi wanachama.
Nilipata fursa ya kuwa kati ya waandishi watano waliowakilisha Tanzania
kwenye mafunzo hayo yaliyolenga kuwanoa wanahabari namna ya kuandika
habari za machafuko na migogoro bila kuleta madhara kwa jamii.
Pamoja na mafunzo, waandishi wa habari kutoka Tanzania walipata fursa ya
kutembelea ubalozi wa Tanzania nchini Burundi. Walipata fursa ya
kujifunza mambo kadhaa, mojawapo ni fursa za uwekezaji zinazopatikana
nchini Burundi.
Katika mazungumzo yake na ujumbe wa waandishi wa habari kutoka Tanzania,
Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk James Mwasi Nzagi pamoja na
mengine alizungumzia fursa ambazo Watanzania wanapaswa kuzichangamkia
hivi sasa.
Uwekezaji katika sekta ya elimu, hasa lugha ya Kiswahili
Burundi ikiwa moja ya nchi zinazoongea lugha ya Kifaransa na Kirundi
kama lugha rasmi ya kiofisi na mawasiliano, imeanza kutilia mkazo lugha
za Kiswahili na Kiingereza ambazo ni lugha rasmi ya mawasiliano ndani ya
EAC.
Serikali ya Burundi hivi sasa inahimiza wananchi wake kujifunza na
kumudu lugha za Kiswahili na Kiingereza. Lugha hizo zinapaswa
kufundishwa kuanzia elimu ya msingi, sekondari hadi Chuo Kikuu.
Katika miaka ya hivi karibuni, Tanzania imekuwa ikizalisha idadi kubwa
ya wahitimu katika sekta ya elimu kuanzia ngazi ya cheti, diploma na
shahada.
Uzalishaji nishati ya umeme
Baada ya kumalizika kwa vita na machafuko, nchi ya Burundi hivi sasa
inaelekeza nguvu nyingi kwenye kujenga na kuinua uchumi wa Taifa hilo
kwa kuhimiza uwekezaji katika sekta ya viwanda, hasa vya uzalishaji.
Hata hivyo, juhudi hizo za serikali zinakwamishwa kwa kukosekana kwa
nishati ya umeme ya uhakika, hali inayofanya viwanda vingi kutumia umeme
unaozalishwa kwa kutumia jenereta.
Matumizi ya umeme wa jenereta hunasababisha bei ya bidhaa za viwandani
kuwa kubwa kiasi cha kupunguza uwezo wa ununuzi kwa wananchi wa kawaida
wa Burundi wanaokadiriwa kuwa zaidi ya 9 milioni.
Huduma katika sekta ya hoteli za kitalii na kumbi za mikutano
Kutokana na kukua kwa kasi kwa uchumi wa Burundi na uwepo wa mikutano ya
kimataifa na wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa na mabalozi wa nchi
mbalimbali, ujenzi wa hoteli za kitalii nchini humo, hasa Mji Mkuu,
Bujumbura umeanza kwa kasi na hivyo kusababisha uhaba wa wafanyakazi
wenye ujuzi.
Sekta ya usafirishaji wa anga, barabara, reli na majini
Burundi ina mikoa 17 ambayo yote imeunganishwa kwa barabara ya lami na
hivyo kutoa fursa ya uwekezaji katika sekta ya usafirisha wa mizigo na
abiria kwa gharama nafuu.
Barabara za lami ambazo zote zimeunganishwa na Mji Mkuu, Bujumbura ni
fursa nyingine ya kibiashara kati ya mikoa mingine, wilaya na vijiji vya
Burundi kwa Watanzania wanaofanya biashara ya usafirishaji abiria na
mizigo kwa njia ya barabara.
Usafiri wa Anga
Hadi sasa hakuna ndege zinazofanya safari ya moja kwa moja kutoka
Bujumbura hadi Jijini Dar es Salaam ambapo abiria wote hulazimika ama
kupitia Nairobi Kenya, Kampala Uganda au Kigali Rwanda ndipo waweze
kufika Dar es Salaam au miji mingine nchini.
Usafiri wa maji (meli)
Tanzania na Burundi zinaunganishwa na Ziwa Tanganyika na hivyo kutoa
fursa ya uwekezaji kwenye sekta ya usafirishaji kwa njia ya maji.
Hivi sasa meli pekee inayotoa huduma ya usafiri kati ya Burundi na Tanzania ni Mv Liemba ambayo umri wake ni zaidi ya miaka 50.
Sekta ya Gesi, hasa za hospitalini
Kuna tatizo la upatikanaji wa uhakika wa gesi za hospitalini ambapo
wakati mwingine taifa hilo hulazimika kupata huduma hiyo kutoka nchini
Kenya.
Kutokana na Tanzania kufanikiwa kuwa na utajiri mkubwa wa nishati ya
gesi, hii ni fursa nyingine ya uwekezaji na kibiashara kwa Watanzania
wenye uwezo, ujuzi, utaalamu na uzoefu katika biashara hii kujitanua
katika soko la Burundi.
Uwekezaji katika viwanda vya Saruji
Hadi sasa, hakuna kiwanda cha Saruji nchini Burundi. Saruji yote
inayotumika nchini humo huagizwa kutoka nje ya nchi na hivyo kufanya
saruji kuwa moja ya bidhaa adimu na muhimu.
Kiwanda cha kutengeneza vyuma
Vyuma vyote vinavyotumika Burundi huagizwa kutoka nje ya nchi, hasa
nchini Ukraine. Mfanyabiashara atakayejenga kiwanda cha chuma atakuwa na
uhakika wa soko.
Kiwanda cha kutengeneza viatu
Kama ilivyo kwa nchi nyingi za Kiafrika, suala la utengenezaji na uvaaji
wa viatu nchini Burundi bado liko katika viwango visivyoridhisha na
siyo ajabu kukuta watu wazima wakitembea pekupeku katika mitaa ya mji
mkuu wa Bujumbura.
Siyo kwamba wananchi nchini Burundi wanatembea peku kwa kupenda. La hasha!
Bei ya viatu iko juu kiasi kwamba wananchi wenye kipato cha chini
hushindwa kumudu kununua viatu ambavyo vingi huagizwa kutoka nje ya
nchi.
Hii ni fursa mwafaka kwa Watanzania wenye uwezo kuwekeza kwenye eneo
hili kwani siyo tu watajihakikishia soko la Burundi lakini pia wataweza
kujipenyeza hadi kwenye soko la nchi jirani ya Rwanda ambako tayari Rais
wake, Paul Kagame amepiga marufuku watu kutembea peku katika mitaa ya
mji mkuu, Kigali.
Kushika soko la Burundi ni njia ya kuingia soko la DRC.
Kutoka mji mkuu wa Burundi, Bujumbura hadi mpakani na nchi jirani ya
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ni chini ya Kilomita 20 pekee.
Ukaribu huu unafanya wafanyabiashara nyingi kuingiliana kati ya Burundi
(Bujumbura) na DRC na hivyo kuongeza fursa za kibiashara kwa Watanzania
watakaowekeza Burundi.
Baadhi ya taarifa muhimu
Ukubwa wa nchi na idadi ya watu:
Nchi ya Burundi iliyopata uhuru Julai Mosi, 1962, ina ukubwa wa kilomita za mraba 28,000 na idadi ya watu zaidi ya 8 milioni.
Makabila Makuu Burundi
Wahutu: Hili ndilo kabila linaloongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watu
nchini Burundi kama ilivyo nchini Rwanda. Inakadiriwa kuwa kabila hili
ni asilimia 85 ya wananchi wote Burundi.
Kiasilia, Wahutu ni Wabantu ambao hujihusisha na kilimo kama njia kuu ya kipato pamoja na ufugaji kwa kiwango kidogo.
Watutsi: Hili ni kabila linalofuata kwa uwingi wa watu nchini Burundi
ikiwa na asilimia 14 ya wakazi wote wa nchi hiyo. Asili yao ni ufugaji
ingawa pia wanashiriki shughuli za kilimo.
Watwa: Hili ni kabila dogo lenye asilimia moja tu ya wakazi wa Burundi ingawa ndilo kabila la watu wa asili nchini humo.
Kiasilia Watwa ni wawindaji, warina asali na waokota matunda (hunters
and gatherers) kama walivyo makabila ya Wahadzabe, Wandorobo, Wasandawe
kwa hapa Tanzania.
Chakula: Chakula kikuu nchini Burundi ni ugali na matoke inayoliwa kwa
nyama, mboga za majani na samaki wanaopatikana Ziwa Tanganyika, hasa
mukake ambao kwa Tanzania, hasa kwa wakazi wa mikoa ya Kigoma, Rukwa na
Katavi hujulikana kwa jina la migebuka.
Burundi pia imejaaliwa kuwa na uwingi wa aina mbalimbali za matunda na
vyakula vitokanavyo na mizizi kama mihogo, viazi vitamu na viazi
mviringo.
Kilimo:Mazao ya kilimo na chakula Burundi ni pamoja na kahawa, pamba, chai, mahindi, mtama, ndizi na viazi vitamu.
Muziki:Muziki maarufu unaopendwa na wananchi Burundi ni ngoma ya
Karyenda ambayo huchezwa kwa mtindo wa kuvutia ukishirikisha wanawake na
wanaume.
Ukiwa Burundi ekupa kuuliza zilipo kambi za jeshi au ofisi za usalama.
Tofauti na Tanzania ni kawaida kumsikia mtu akisema kambi ya jeshi ya
Mgulani, oohh Morogoro kuna kambi ya mizinga n.k. Aidha, huruhisiwi
kupiga picha mitaani bila kibali cha Meya wa mji, kwa sababu za
kiusalama.
Mwananchi
No comments:
Post a Comment
Toa maoni yako lakini angalia kuchafua hali ya hewa na usimuumize mwenzako