Na Bin Zubery
NDOTO
za Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’ kurudia kile ilichokifanya mwaka
1994 nchini Kenya katika Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati,
CECAFA Challenge ziliyeyuka jana usiku baada ya kufungwa 1-0 na wenyeji,
Harambee Stars Uwanja wa Nyayo, Nairobi, bao pekee la mshambuliaji wa
Thika United, Clifton Miheso dakika ya nne kwa shuti la umbali wa mita
20, baada ya kupokea pasi fupi ya Alan Wanga na kumchungulia kipa Ivo
Mapunda.
Stars
sasa itawania nafasi ya tatu kwa mara ya pili mfululizo kwa kumenyana
na Zambia ambayo nayo jana ilifungwa 2-1 na Sudan katika Nusu Fainali
nyingine Uwanja wa County ya Mombasa, zamani Manispaa.
Hii
ni mara ya pili mfululizo, kocha Mdenmark, Kim Poulsen anaiongoza Stars
katika Challenge bila ya mafanikio, baada ya mwaka jana pia mjini
Kampala, Uganda kufungwa katika Nusu Fainali na wenyeji, Uganda.
Matokeo
haya yanakuja, wakati tayari Kim ameshindwa kuiwezesha timu ya
Tanzania, Taifa Stars kufuzu kushiriki mashindano yoyote kati ya
iliyowania tiketi zake tangu arithi mikoba ya Mdenmark mwenzake, Jan
Poulsen Mei mwaka jana.
REKODI YA KIM POULSEN STARS
Mei 26, 2012
Tanzania 0 – 0 Malawi (Kirafiki)
Juni 2, 2012
Ivory Coast 2 – 0 Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 10, 2012
Tanzania 2 – 1 Gambia (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 17, 2012
Msumbiji 1 – 1 Tanzania (Tanzania ilitolewa kwa penalti kufuzu Mataifa ya Afrika)
Agosti 15, 2012
Botswana 3 – 3 Tanzania (Kirafiki)
Novemba 14, 2012
Tanzania 1-0 Kenya (Kirafiki)
Desemba 22, 2012
Tanzania 1-0 Zambia (Kirafiki)
Januari 11, 2013
Tanzania 1-2 Ethiopia (Kirafiki)
Februari 6, 2013
Tanzania 1-0 Cameroon (Kirafiki)
Machi 24, 2013
Tanzania 3-1 Morocco (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 2, 2013
Sudan 0 – 0 Tanzania (Mechi ya kirafiki Ethiopia)
Juni 8, 2013
Morocco 2-1 Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 6, 2013
Tanzania 2-4 Ivory Coast (Kufuzu Kombe la Dunia)
Julai 13, 2013
Tanzania 0-1 Uganda (Kufuzu CHAN)
Julai 27, 2013
Uganda 3-1 Tanzania (Kufuzu CHAN)
Septemba 7, 2013
Gambia 2-0 Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
...KOMBE LA CECAFA CHALLENGE Novemba 25, 2012 Tanzania 2–0 Sudan (Kundi B) Novemba 28, 2012 Tanzania 0–1 Burundi (Kundi B) Desemba 1, 2012 Tanzania 7-0 Somalia (Kundi B) Desemba 3, 2013 Tanzania 2-0 Rwanda (Robo Fainali) Desemba 6, 2012 Tanzania 0–3 Uganda (Nusu Fainali) Desemba 8, 2012 Tanzania 1-1 Zanzibar (Zanzibar ikashinda penalti 6-5) Novemba 28, 2013 Tanzania 1-1 Zambia (Kundi B) Desemba 1, 2013 Tanzania 1-0 Somalia (Kundi B) Desemba 4, 2013 Tanzania 1-0 Burundi (Kundi B) Desemba 7, 2013 Tanzania 2-2 Uganda (Robo Fainali, Stars ikashinda kwa penalti 3-2) Desemba 10, 2013 Tanzania 0-1 Kenya (Nusu Fainali)
...KOMBE LA CECAFA CHALLENGE Novemba 25, 2012 Tanzania 2–0 Sudan (Kundi B) Novemba 28, 2012 Tanzania 0–1 Burundi (Kundi B) Desemba 1, 2012 Tanzania 7-0 Somalia (Kundi B) Desemba 3, 2013 Tanzania 2-0 Rwanda (Robo Fainali) Desemba 6, 2012 Tanzania 0–3 Uganda (Nusu Fainali) Desemba 8, 2012 Tanzania 1-1 Zanzibar (Zanzibar ikashinda penalti 6-5) Novemba 28, 2013 Tanzania 1-1 Zambia (Kundi B) Desemba 1, 2013 Tanzania 1-0 Somalia (Kundi B) Desemba 4, 2013 Tanzania 1-0 Burundi (Kundi B) Desemba 7, 2013 Tanzania 2-2 Uganda (Robo Fainali, Stars ikashinda kwa penalti 3-2) Desemba 10, 2013 Tanzania 0-1 Kenya (Nusu Fainali)
Taifa
Stars chini ya Kim, kwanza ilitolewa kwenye kuwania tiketi ya kucheza
Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON), ikatolewa pia kwenye
kinyang’anyiro cha Kombe la Dunia na ikatolewa pia kwenye kinyang’anyiro
cha tiketi ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN).
Nakumbuka,
wakati anapewa timu, Kim alisema lengo lake ni fainali zijazo za
Mataifa ya Afrika- alikuwa sahihi kwa sababu wazi angehitaji muda
kutengeneza timu na kuiandaa kwa ujumla.
Lakini
kulingana na mwenendo wenyewe na hali halisi ya timu kwa ujumla, chini
ya Kim huwezi kuona dalili za Tanzania kupata tiketi ya Fainali zijazo
za AFCON. Neno rahisi ni kwamba mwenendo wa timu yetu mbele ya Kim si
mzuri, kiasi kwamba hata yeye mwenyewe anaonekana kabisa kuanza kukata
tamaa.
Mbaya
zaidi, hata wadhamini wa timu, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) nao
wanaonekana kuanza kukatishwa tamaa na timu hiyo chini ya Kim- si hadi
Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe aseme, lakini
dalili zinaonekana.
Mwaka
jana katika Challenge ya Uganda, TBL walituma mwakilishi wake kuwa bega
kwa bega na timu kama ambavyo wamekuwa wakifanya kwenye mechi zote,
lakini safari hii hawakuwa tayari kuchoma moto fedha zao kwa ajili ya
timu ya Kim.
Nimesema
mbaya zaidi wadhamini wanaonekana kuanza kukatishwa tamaa na timu yetu
ya taifa pia chini ya kocha Kim, kwa sababu udhamini ndiyo uti mgongo wa
timu, bila ya hivyo hali itakuwa mbaya zaidi na timu hiyo itakuwa mzigo
kwa kila mtu.
Achana
na madudu haya ya CECAFA Challenge, hadi sasa kocha Kim ameiongoza timu
yetu ya taifa, Taifa Stars katika mechi 16 na kuambulia ushindi katika
mechi tano, kufungwa saba na sare nne.
Inauma
zaidi tulifungwa na Uganda nyumbani na ugenini kuwania tiketi ya CHAN
na kila siku Kim amekuwa akilia na wachezaji na amekuwa akibadilisha
vikosi mara kwa mara. Ameachana na makipa aliokuwa nao tangu aanze kazi,
Juma Kaseja na Mwadini Ally na kuwachukua Ivo Mapunda na Deo Munishi
‘Dida’ na amekuwa akibadilisha wachezaji atakavyo. Hakuna
anayemuingilia, kwa sababu watu wanataka matokeo tu.
Sasa
jitihada zake zote, matokeo yake ndiyo haya ambayo tunayaona sasa na
huwezi kusema kingine, hata kama Kim ni kocha bora kiasi gani, mchapa
kazi wa aje, kwa kuwa matokeo ya timu yetu si mazuri, basi hatufai.
Binafsi, nampenda Kim, napenda sera zake napenda namna anavyofanya kazi.
Jamaa ni hodari sana. Lakini sioni matunda ya kazi yake!
Rejea
CECAFA Challenge ya mwaka huu, Kim atatoa kisingizio gani? Aliita timu
mbili zikawekwa kambini zote, timu ya chipukizi, Future Taifa Stars na
ya wakubwa, Taifa Stars ambazo baadaye zilimenyana ili ateue wachezaji
wa kuja nao Challenge. Kutokana na mechi ambayo Future waliwafunga kaka
zao 1-0, Kim akateua kikosi cha Challenge.
Bahati
iliyoje kwake, TP Mazembe nayo ikawaruhusu Mbwana Samatta na Thomas
Ulimwengu kuja kuichezea timu ya Kim- kwa hivyo alipata kila
alichokihitaji na matokeo yake tukafungwa 1-0 katika mchezo ambao
tungeweza kushinda kama si upangaji wake wa timu usioeleweka. Kuna
wachezaji anawang’ang’ania kikosini huwezi kuona kwa sababu gani, wakati
anawaacha wachezaji bora.
Tazama
mabadiliko aliyoyafanya jana, alimtoa Amri Kiemba akamuingiza Farid
Mussa, ambaye alishindwa kabisa kucheza, kila pasi akipelekewa ilikuwa
mpira unatoka nje. Lakini ukirejea nyuma, kuna wachezaji ambao tayari
Kim alikwishaanza kuwajengea kujiamini katika mashindano haya tangu
hatua ya makundi, akina Haroun Chanongo na Ramadhani Singano ‘Messi’ na
ambao pia wanamzidi uzoefu Farid.
Kufungwa
si kitu, suala ni namna ambavyo mnafungwa- Chanongo alimfungia bao Kim
katika mechi na Somalia na bado ameonekana kucheza vizuri akiwa pamoja
na Messi, jana baada ya kuona aliowategemea wameshindwa, kwa nini
asiwaingize hao vijana?
Ile
ilikuwa mechi kubwa, Kim alimuonea Farid na mbaya zaidi kwa sababu
mechi ilikuwa imekwishachafuka- afadhali angemuingiza katika mchezo
ambao Stars ilikuwa inaongoza. Sasa, matokeo yake badala ya kumjenga
mchezaji huyu chipukizi mwenye kipaji, Kim anajikuta anachangia
kumbomoa. Wachezaji wadogo huwa wanainuliwa taratibu na si kama
anavyotaka kufanya Kim.
Lakini
pamoja na yote, bado huwezi hata kufurahishwa na mfumo wa uchezaji wa
Stars, ndiyo kuna wakati zinapigwa hata pasi thelathini, lakini zisizo
na malengo wala mipango zaidi unaweza kuona mabao yanatokana na juhudi
binafasi za wachezaji. Kwa kweli bila kuoneana haya, Kim ni rafiki yetu,
na abaki kuwa rafiki yetu, lakini hafai kuendelea kuwa kocha wa timu
yetu. Jumatano njema.

No comments:
Post a Comment
Toa maoni yako lakini angalia kuchafua hali ya hewa na usimuumize mwenzako