A

A

NEY WA MITEGO ATOA MACHOZI USIKU KUCHA JUU YA MTOTO WAKE


JAMBO limezua jambo! Siku chache baada staa wa Bongo Fleva, Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’ kudaiwa kumfumania mpenzi wake Siwema Edson kisha kuondoka na mtoto wa miezi mitatu (Curtis), mrembo huyo ameibuka na kudai mtoto huyo si mali ya Mbongo Fleva huyo hali ambayo imesababisha mama yake mzazi Nay apate mshtuko, Ijumaa Wikienda linakupa mchapo hatua kwa hatua.

Ijumaa iliyopita, gazeti tumbo moja na hili la Ijumaa liliripoti tukio la Nay kutonywa kuwa mchumba’ke anachepuka jijini Mwanza anakoishi ambapo Nay aliamua kufunga safari kutoka Dar hadi Mwanza na kumfumania Siwema akiwa na ‘serengeti boy’ wake.

HABARI YAMTIBUA SIWEMA

Mara baada ya habari hiyo kupeperuka hewani, rafiki wa karibu na Siwema alimvutia waya mwanahabari wetu ambapo alieleza jinsi gani Siwema amechukizwa na habari hiyo.

TUJIUNGE NA SHOSTI

“Nilikuwa na Siwema, kusema kweli amemlalamikia sana Nay, anasema tangu alipokuwa mjamzito alikuwa na mgogoro mkubwa sana na Nay, hata alipojifungua amekuwa akivumilia vitu kibao kutoka kwa jamaa (Nay)

ETI HALIKUWA FUMANIZI

“Zaidi alichokuwa akilalamikia Siwema ni juu ya Nay kusema alimfumania wakati siku hiyo yeye alimkuta anamnyonyesha mwanaye, hata anaposema kamkuta na mwanaume, haoni hoja ya Nay kusema hilo wakati mwenyewe alimwambia hamtaki na kumruhusu kutafuta bwana sasa amemkuta analalamika nini tena?

KIGOGO AMPA JEURI SIWEMA

“Kwanza Siwema ana kigogo wake serikalini ndiye anayempa jeuri, sasa sijui hata anamfuatafuata wa nini,” alisema rafiki huyo.

SIWEMA ANASEMAJE?

Baada ya kunasa mazungumzo hayo ya shosti huyo, mwanahabari wetu alimsaka Siwema mwenyewe ili kujua anazungumziaje sakata hilo, alipopatikana, alifunguka:

“Yaani we acha tu katika maisha huwa kuna siri sana, najua watu wengi wanaongea mambo ambayo hawayajui vizuri, nimeanza uhusiano na Nay siku nyingi sana na kote huko mimi mambo yangu yalikuwa safi kuliko yeye ambaye hata jina alikuwa hana, namshangaa sana leo maneno anayoropoka kwa watu eti alinifumania wakati siku anakuja kwangu alinikuta nimembeba mwanangu Curtis na nilikuwa namnyonyesha, nafikiri ajaribu kumuogopa Mungu kidogo.

AZIDI KUFICHUA MAOVU

“Kuna uchafu mwingi sana alikuwa akinifanyia na hata hivyo kusema kanihonga gari, ni muongo kwani hili gari (Toyota Mark X) ni langu, hakumbuki zile Toyota Lexus na Toyota Verossa zangu nilizompa? Amenirudisha nyuma sana kimaisha hata mama na dada yake anajua haya, tangu nimekuwa naye mimi ndiyo mkosaji tu? Mimi huyuhuyu ndiye nilikuwa nikimuomba msamaha kila kukicha hadi mwisho akanitamkia nitafute boyfriend, hata hilo bado hakumbuki na kuendelea kuongea vya uongo?”

APIGILIA MSUMARI WA MTOTO

“Najua kweli ana watoto zaidi ya watatu nafikiri hata hao wengi bado ana muda wa kuwataja tu na wajulikane kwenye jamii asijifanye anampenda sana Curtis, amuache tu maana si wake mimi ndiye ninayeweza kujua zaidi baba wa mtoto na asijifanye kimbelembele na kutaka kunichafulia kwenye jamii wakati ukweli naujua mimi,” alisema Siwema.

MAMA APATA MSHTUKO

Kufuatia habari hiyo ya Nay kumfumania Siwema na mchumba huyo wa mwanaye kufunguka kuwa mtoto si wa Nay, chanzo kilicho karibu na familia ya msaanii huyo kimepenyeza habari kuwa mama mzazi wa Nay, Matlida Mwaipopo alipata mshtuko na kushindwa kuzungumzia suala hilo.

“Mama Nay amepata mshtuko mkubwa, presha imepanda na hapa tunavyoongea na wewe, tumejaribu kumtuliza ili aweze kusaidia tatizo hili kifamilia, ameshindwa kuzungumzia lolote,” kilisema chanzo hicho.

NAY ALIA USIKU KUCHA

Alipotafutwa Nay kuhusina na tukio hilo, alishindwa kuzungumzia lolote zaidi ya kulia kutwa na hata alipotafutwa baadaye bado alizungumza huku akilia.

“Suala la kuambiwa mtoto si wangu linaliza na hadi muda huu naumia sana, inafikia wakati nashindwa hata niseme nini ila anachokitaka kwangu atakipata, wewe mwacheni aendelee kuropoka na kunidhalilisha huko Instagram, ukweli mimi sina neno naye na zaidi nimechukua mtoto wangu na nawapenda sana wanagu wote,” alisema Nay na hata alipotafutwa usiku sana siku hiyo (Ijumaa iliyopita), bado alisikika akilia kwa uchungu.

KIKAO CHA FAMILIA CHAANDALIWA

Wakati gazeti hili linakwenda mitamboni, chanzo makini kilivujisha habari kuwa kuna baadhi ya ndugu wa karibu wa Nay wanaandaa kikao cha familia ili kutafuta suluhu ya jambo hilo.

“Kuna kikao kizito kinaandaliwa cha familia kutafuta suluhu lakini tutakujuza zaidi kitakapofanyika,” kilisema chanzo hicho.

SOURCE: GPL

No comments:

Post a Comment

Toa maoni yako lakini angalia kuchafua hali ya hewa na usimuumize mwenzako